27/03/2021
CHAMA CHA MAPINDUZI KINAPOMTAFUTA MAKAMU WA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, NAOMBA NIWAKUMBUSHE YAFUATAYO:
Ndugu Wana Ccm,
Kufuatia kifo cha aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli hivi karibuni, na aliyekuwa Makamu wake Mama, Samia Suluhu Hassan kuapishwa kushika madaraka ya Rais kukidhi matakwa ya Kikatiba Ibara ya 37 (5), hivi sasa Chama chetu kipo kwenye mchakato wa kumpata Makamu wa Rais mwingine kutoka miongoni mwa makada wake wenye sifa.
Uzoefu unaonyesha kwamba, kwenye hatua hii kuna kila dalili zenye kuonyesha uwezekano wa kuibuka kambi mbili, kati ya kambi iliyoko madarakani inayopigania kuendelezwa kwa falsafa yake ya hapa kazi tu dhidi ya kambi mtandao inayopambana kuweka mtu wake atakayetetea maalshi yao. Kimsingi mchakato huu unaweza kupelekea kukipasua chama vipande vipande.
Wakati mchakato huu wa kumpata Makamu wa Rais ukiendelea ndani ya Chama, huku ukishirikisha viongozi wastaafu wenye ushawishi ndani ya Chama na serikali, naomba nitowe angalizo, kusije kukafanyika makosa nchi ikarudi mikononi mwa wezi, wala rushwa, mafisadi, wapiga dili, waporaji wa rasilimali, majambazi pamoja na kushamiri kwa dawa za kulevya, hali iliyopelekea Ccm kunuka, kuchokwa pamoja na kuchukiwa na wananchi waliokata tamaa kiasi cha kutamani kuongozwa na shetani, na k**a si kumteua mgombea aliyekubalika na wananchi, Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na kuwa na mfumo wa uchaguzi unaoinufaisha Ccm, ingeondoka madarakani mwaka 2015.
Ndugu Wana Ccm,
K**a mmesahau, naomba niwakumbushe kwamba, Baba wa taifa Mwl. Julius Kambarage Nyerere alipostaafu (kung'atuka) madarakani mwaka 1985, aliliacha taifa likiwa moja, lenye mshik**ano, japokuwa tuliyumba kiuchumi kutokana na athari za vita vya Kagera, pale majeshi ya Nduli Iddi Amin Dada yalipoivamia nchi yetu na kuteka sehemu ya ardhi ya Mkoa wa Kagera.
Katika swala la uongozi wa nchi, tulikuwa na Azimio la Arusha lililokuwa na misingi ya utu, ikiwemo miiko ya viongozi ambayo pamoja na mambo mengine, lilipiga marufuku viongozi kujilimbikizia mali au fedha kwa njia isiyo halali.
Rais wa awamu ya pili, Mhe. Ally Hassan Mwinyi alipoingia madarakani, kupitia kauli mbiu yake ya Ruksa, kikaitishwa kikao cha Halmashauri kuu ya Taifa (Ccm) kilichofanyikia huko Zanzibar kwa ajili ya kuhuisha Azimio la Arusha, ambapo walikuja na Azimio jipya la Zanzibar lililofuta miiko ya viongozi kujilimbikizia mali na fedha kwa njia haramu, na kuanzia hapo ndipo rushwa na ufisadi ilipozaliwa, na Ccm ikaanza kufungamana na matajiri badala ya kutetea wananchi wanyonge na masikini.
Ni kuanzia wakati huo, uongozi ulipogeuka kuwa biashara badala ya kutumikia watu. Kutokana na kulinda masilahi yao, wafanya biashara wenye ukwasi wa fedha wakatumia fursa hiyo kununua nafasi mbali mbali za uongozi kwenye Chama, na hata kudiriki kugombea nafasi za kisiasa k**a Ubunge, Udiwani, na miongoni mwao wakafanikiwa kuteuliwa kuwa viongozi wa serikali ikiwemo Mawaziri, Wakuu wa Mikoa nk. Ni kuanzia wakati huo, Ccm na serikali yake ilipoacha kusikiliza na kutatua kero za wananchi, ukwepaji kodi dhidi ya wafanya biashara ukaanza kutokana na Chama kutegemea wafanya biashara kukifadhiri kipindi cha uchaguzi.
Alipoulizwa Rais Mwinyi, baada ya mambo kuharibika, kwa nini alivunja Azimio la Arusha na badala yake kuja na Azimio la Zanzibar, alijibu kuwa, walipofungua milango na madirisha ili hewa safi iingie, hawakujua kuwa, mbu, vumbi na inzi nao wangeingia kwa pamoja.
Ndugu Wana Ccm,
K**a vile Chama hiki kilikuwa na laana ya Baba wa taifa, hata baada ya Rais Mwinyi kumaliza mihula yake miwili madarakani kwa mujibu wa Katiba, na kukabidhi kijiti kwa Rais Benjamin William Mkapa, hakikutaka kujirekebisha, bali mambo ndivyo yalizidi kuharibika zaidi.
Kupitia kauli mbiu ya Ukweli na Uwazi, Serikali ya Rais Mkapa ilifanya ubinafsishaji wa mashirika ya umma karibu yote, yakiwemo yaliyokuwa yakijiendesha kwa faida k**a vile Benki ya NBC, Kiwanda cha Sigara, nyumba za serikali zikauzwa, huku viongozi wa serikali wakigeuka kuwa wateja kwa kujiuzia sehemu ya mashirika hayo kwa bei ya kutupwa ikiwemo migodi. Watu wakakosa ajira, uchumi ukaanguka.
Ni kupitia serikali hii ya Mkapa, viongozi kwa kushirikiana na wafanya biashara walipoanza kukwapua fedha za umma ikiwemo Akaunti ya madeni ya nje EPA. Katika hili, hakuna aliyewajibishwa mpaka leo, licha ya Mkapa kuomba radhi kupitia kitabu alichokiandika baada ya kutoka madarakani.
Ndugu Wana Ccm,
Wahenga wa kale walisema, sikio la kufa kamwe huwa halisikii dawa. Hivyo ndivyo hali ilivyokuwa mwaka 2005, pale Rais wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alipoingia madarakani kwa mbwembwe kupitia kauli mbiu yake ya Ari mpya, Nguvu mpya, Kasi mpya, na Maisha bora kwa kila Mtanzania.
Kwa namna alivyokuwa amejipanga, na kwa jinsi alivyowaaminisha wananchi (Wapiga kura), waliamini ujio wa Rais Kikwete ndiye alikuwa suluhisho la matatizo yao ikiwemo huduma mbovu za afya, ukosefu wa maji safi na salama, anguko la elimu kwenye shule za serikali, mgao wa umeme usio na kikomo nk.
Kinyume chake, kilichotokea ni kwamba, kauli mbiu ya Ari mpya, Nguvu mpya, Kasi mpya, na Maisha bora kwa kila mtanzania, ilitafsiriwa kwa vitendo vya rushwa kuongezeka zaidi, kuongezeka kwa ufisadi kupitia mikataba ya uwekezaji ukiwemo mkataba wa kufua umeme wa dharula wa Richimond/Dowans achilia mbali ukwapuaji wa fedha Bilioni 306 za akaunti ya Escrow kati ya Tanesco na Benki ya Standard Chaterd, ambazo inaelezwa waliozikwapua baadhi yao walibeba kupitia viroba vya sandarusi.
Ndugu Wana Ccm,
Wakati haya yakifanyika, hakuna paka aliyeweza kumfunga kengele paka mwenzake. Rushwa kwenye taasisi za serikali ikiwemo zinazotoa huduma ikageuka kuwa ibada. Si Polisi, Mahak**a, Hospitali wala Mamlaka ya Mapato, au Uhamiaji. Kote huko kulinuka rushwa. Watu wakaanza kuabudu fedha. Wenye fedha ndiyo wakawa na sauti ya kusikilizwa kila mahali, na hata kuituma setikali. Masikini na wanyonge wakakosa mtetezi. Dawa hospitalini zikawa bidhaa adimu. Aliyeugua huku akiwa hana fedha, huyo niagieni au kwa neema ya Mungu amnusuru. Wajawazito wakalala sakafuni, wengine mzungu wa nne, huku kujifungua wakilazimika kwenda na vifaa vyao. Kutokana na hali ilivyokuwa mbaya, mwanamke kubeba mimba na kwenda kujifungulia hospitali za umma ikawa ni kuomba, ama kubaki hai duniani au kwenda ahera.
Kwenye swala la elimu, huku ndiko hali ilikuwa mahututi kabisa. Tangia baba wa taifa alipong'atuka madarakani, shule zilitekekezwa. Hakuna darasa jipya lililojengwa, hakuna matundu mapya ya vyoo yaliyojengwa, hakuna nyumba mpya ya mwalimu iliyojengwa kukabili upungufu, wala hakuna dawati jipya lililotengenezwa. Matokeo yake ni wanafunzi kukaa sakafuni, kwenye mawe, kwenye vipande vya matofali huku kila mwaka wazazi wakichangishwa fedha ya ujenzi wa vyumba vya madarasa, vyoo na madawati, lakini hakuna kilichofanyika, tofauti na k**ati za shule kujineemesha. Wakati haya yanafanyika, Ccm ipo, na serikali yake ipo lakini imefumba macho na kuziba masikio.
Nchi ilivyoonekana k**a vile haina mwenyewe, ni shamba la bibi, kila mtu akaamua kuchukua chake mapema. Majambazi kwa upande wao kazi ikawa ni kupora fedha benki kwa mtutu wa bunduki mchana kweupe, achilia mbali watekaji magari usiku, walioifanya serikali kusalimu amri kwa kuzuia mabasi kusafiri usiku baada ya saa 4. Hali ilikuwa vivyo hivyo kwenye ajali madereva wakishindana kuuwa abiria.
Ndugu Wana Ccm,
Ukienda kwenye ujangiri ndo usiseme ambapo tunaambiwa muuwaji wa tembo raia wa China aliyejipachika jina la malikia wa tembo, alianza kuuwab embo tangu mwaka 1986, hakuk**atwa, lakini akaja kuk**atwa Decemba 2015 baada ya Rais Magufuli kuingia madarakani. Hiyo ni tisa, kumi ni pale ndege ya Jeshi ya nchi nyingine ilipotua na kubeba twiga.
Katika eneo la kukwepa kodi, unaambiwa meli zilishusha mafuta pasipo mafuta hayo kupitia kwenye mita licha ya kwamba mita zilikuwepo. Mwenye meli ndiye alitoa taarifa kwa mamlaka ameshusha kiasi fulani, baasi. Ccm ipo, serikali ipo k**a vile imewekwa mfukoni.
Ndugu Wana Ccm,
Nataka niwaonye viongozi wanaoshiriki mchakato wa kumpata Makamu wa Rais ndani ya Ccm kwamba, iwapo watatanguliza maslahi yao mbele badala ya maslahi ya taifa, watambuwe kuwa, miaka hii mitano ndiyo itakuwa ya mwisho Ccm kuongoza.
Hayati Rais Magufuli, licha ya kuaga dunia, mojawapo ya manufaa makubwa tuliyopata kwake, ametutoa usingizini kutambua nchi yetu si masikini bali ni tajiri. Wimbo wa umasikini tulioimbiwa miaka nenda rudi ilikuwa ni kiini macho cha viongozi wetu kujilimbikizia mali nabfedha huku wananchi tukibakia hohe hahe. Kwa msingi huo, endapo Ccm itakosea, ikampitisha Makamu wa Rais miongoni mwa wapiga dili, itambuwe kuwa, uchaguzi wa mwaka 2025 utakuwa nj uchaguzi muhimu kuliko chaguzi zote zilizowahi kufanyika. Tutapiga kura kuchagua viongozi tukiwa na uelewa mkubwa kuhusu ni kiongozi gani anatufaa. Hayati Rais Magufuli ametufundisha umuhimu wa kulinda na kutetea rasilimali zetu.
Ndugu Wana Ccm,
Naomba nihitimishe kwa kusema kwamba, nchi yetu ilipokuwa imefikia kwa viwango vya maovu vilivyofumbiwa macho na masikio na serikali, tulihitaji uongozi/kiongozi mwenye kariba aina ya Magufuli.
Rushwa ilitamalaki kufikia hatua ya mwananchi wa kawaida kupata haki ni majaaliwa ya mwenyezi Mungu. Ufisadi uliota mizizi kufikia kiwango kwa Chama kujiibia mali zake chenyewe na kuwapa wenye fedha. Ubadhirifu wa fedha za serikali kupitia miradi, vikao, safari, warsha ulikubuhu, huku Ujambazi ukirindima kila kona. Ajali zisizo na kikomo, Uwajibikaji na nidhamu serikalini ziro. Ujangiri usipime. Uporaji rasilimali za nchi ukawa shamba la bibi. Ukosefu wa dawa hospitali. Mgao wa umeme usiokwisha. Ukwepaji kodi. Watumishi hewa. Wenye vyeti feki. Dhuluma dhidi ya wenye haki. Migogoro ya ardhi. Wezi ndiyo walitungiwa nyimbo za kusifiwa. Watu hawakutitii sheria za nchi wala mamlaka kwa kisingizio cha demokrasia na haki za binadamu.
Tunamtaka Makamu wa Rais atakayekuja kupambana nanrushwa, ufisadi, ukwepaji kodi, hatutaki Makamu wa Rais atakayekuja kula bata na kulinda maslahi ya wapiga dili. Kwangu mimi, aina ya uongozi wa Rais Magufuli bado unahitajika kwenye nchi yetu kwa miaka 50 ijayo. By Mpenda Amani, maendeleo na umoja wa kitaifa ukistawishwa na uzalendo wa nchi yetu ya Tanzania! Share ujumbe huu uwafikie Watanzania wote