26/03/2026
RIWAYA: SIKU 4 ZA LOCKDOWN
Mtunzi: Saul David Bril
WhatsApp: 0756862047
SEHEMU YA 40
ILIPOISHIA.....
k**a alivyotarajia.
Aliyesimama mbele yake, akiwa amemkodolea macho ya mshangao alikuwa ni Nisha, mpenzi wa Jordan.
Makuratha alibaki mdomo wazi, aibu na hofu ya kujiachia mbele ya Nisha vilimjaa. Mbaya zaidi alishamwita na jina eti 'Jordan'
SASA ENDELEA....
Ukimya ulitawala pale mlangoni. Makuratha aliona haya. Nisha alimwangalia kuanzia juu mpaka chini, akaona jinsi mwanamke huyo alivyosimama nusu uchi akiwa amevaa taiti pekee mwilini mwake. Hata hivyo, Nisha hakuonesha kushtuka, badala yake alitoa tabasamu la kistaarabu sana, hakujali.
"Hi! tunaweza kuongea kidogo kipenzi?" Alisema Nisha.
Makuratha akaduwaa, macho yake yakitazama huku na kule kwa wasiwasi.
"Ku... kuongea? Hapa?" Makuratha aliuliza huku akijaribu kuweka mkono wake mmoja juu ya matiti yake ili kujisitiri mbele ya mwanamke mwenzake.
"Hapana, siyo hapa mlangoni. Pale panafaa..." Nisha alimuonesha kwa mkono eneo la mapumziko lililokuwa karibu na vyumba hivyo.
Palikuwa na seti nzuri ya sofa, meza ya kioo, na runinga kubwa ukutani. Ni eneo maalum la ghorofa ya kwanza kwa ajili ya wageni kupunga upepo. King G ni hoteli ya kifahari buana.
Makuratha alimeza mate...
"Sa...sawa, ngoja nivae basi, nakuja" Makuratha alisema na kurudi ndani haraka.
Akiwa ndani, alivaa nguo zake huku moyo ukimdunda. Alikuwa na wasiwasi mwingi. Alijiuliza k**a Nisha amemsikia vizuri pale aliposema "My Jordan Surprise" au hakusikia.
Ukweli hakuwa na uhakika jibu lipi ni sahihi, amesikia au hajasikia.
Hata hivyo, asili yake ya ubabe na jeuri ilimrudia.
"Potelea mbali, hata akisikia, kwani nini bana, akizingua namzingua pia. Acha nimsikilize anataka nini" Makuratha aliwaza huku akifunga zipu ya suruali yake. Tayari amemaliza kuvaa.
Alimtazama yule mlinzi kitandani. Mwanaume huyo alikuwa bado amelala fofofo akikoroma mkoromo wa ajabu huku udenda ukimtoka mdomoni na kulowanisha mto aliolalia. Makuratha alimpiga tu jicho la pembeni, wala hakujali hali yake, akatoka nje na kufunga mlango. Hakujua kuidharau hali ile ya mlinzi niko kubwa anafanya. Kosa lenye majuto makubwa hapo baadae.
****
Makuratha alimkuta Nisha ameshakaa kwenye sofa anamsubiri.
Bila salamu wala nini, Makuratha alijitupa kwenye kiti cha pili akaweka pozi kwa namna ya kujiamini sana.
"Nakusikiliza, nikusaidie nini?" Makuratha aliuliza.
Nisha alimtazama kwa jicho la udadisi, akijaribu kumsoma mwanamke huyu, akagundua ana kiburi fulani.
"Naitwa Nisha, binti wa Meya Magi..."
Kabla Nisha hajamaliza kujitambulisha, Makuratha alimkatisha.
"Nakufahamu vizuri Nisha, nenda tu kwenye point moja kwa moja, sina muda please"
Makuratha alikuwa anatafuta shari kwa makusudi kabisa.
Ukweli ni kwamba, anamchukia Nisha kwa moyo wake wote. Sababu kubwa ni wivu wa mapenzi; Makuratha anaamini kuwa Nisha ndiye sababu iliyomfanya Jordan amuache yeye enzi hizo na kumuona sio wa muhimu tena. Hivyo, kumuona Nisha mbele yake ilikuwa ni k**a anamuona adui yake nambali moja kwenye sekta nyeti ya mapenzi.
Nisha alishusha pumzi, akaamua kupuuza jeuri hiyo kutoka kwa Makuratha.
"Vema k**a unanijua. Bila shaka basi unaelewa pia mimi ni nani kwa Jordan, na nina nafasi gani kwake."
Makuratha alicheka kicheko cha kejeli.
"Hahahaha we kuweza... enhe! Nielewe ni nani kivipi? Wewe si ni mwanamke tu k**a nilivyo mimi kwake. Au unajiona nani mwenzangu hebu nambie, malkia au?"
Maneno ya Makuratha yalijaa shombo na dharau za wazi. Lengo lake lilikuwa kumfanya Nisha apaniki, apate hasira, kisha mazungumzo yavurugike.
Lakini Nisha alikwepa mtego huo.
Licha ya kugundua alichokitaka kwa Makuratha hatokipata kutokana na namna alivyompokea, lakini Nisha aliamua kuwa mpole. Hakuelewa ni kwanini mwanamke huyu anamjibu shombo kiasi hicho.
Nisha aliamua kubadili mbinu. Akaona njia pekee ni kumchokoza kwa maneno ili apate ukweli fulani anaouhisi.
Akaanza kwa kusema...
"Nimeona umeingia na mwanaume chumbani kwako muda mfupi uliopita, lakini bado unasema mimi na wewe ni sawa kwa Jordan. Labda sijakuelewa vizuri mrembo. Sawa kivipi? Na huyu mwanaume aliyelala chumbani kwako sasa hivi ni nani? Na Jordan ni nani?"
Swali hilo lilimgusa Makuratha pabaya...
Nisha hakuishia hapo, aliongeza dozi ya pili.
"Umenipokea mlangoni ukidhani mimi ni Jordan, si eti? Tena ukiwa uchi wa mnyama. Jana mmekuja hapa mmevaa nguo za heshima za mapadri na masista, lakini leo mnakaribishana mkiwa uchi. Unaweza kuniambia ni filamu gani mnaigiza? Inaonekana ni kali sana eti eeh?"
Nisha alimsogelea kidogo na kumnong'oneza.
"Yaani una mwanaume ndani chumbani kwako, bado unampokea mwanaume mwingine ukiwa uchi? We dada, mnacheza filamu za ngono eti?"
Maneno hayo yalimchoma Makuratha k**a sindano ya moto. Akajikuta anakosa uvumilivu, na hiki ndicho alichokuwa akikitafuta Nisha. Kumfanya Makuratha apaniki.
"Shika adabu yako Nisha! Kwanza wewe ni nani hadi utake kujua maisha yangu? Kwa nini usimfuate huyo Jordan wako ukamuulize maswali yako ya kijinga?"
Makuratha alisimama, akitaka kuondoka lakini akageuka kumpa Nisha onyo la mwisho.
"Sikiliza wewe, siku ukijua nini Jordan anafanya nyuma ya pazia, nina imani utapasuka kichwa. Labda nikushauri tu, achana na Jordan mapema kabla hujakuua kwa presha, maana si....."
Makuratha hakumalizia sentensi yake. Ghafla aliganda na kutoa macho.
Kule mlangoni alimuona Jordan akija kwa kasi. Hua zake zikiwa ndefu ndefu, akafika mbele ya mlango wa chumba cha Makuratha akasimama.
Mlango ulikuwa umefungwa lakini tayari Jordan alisikia sauti ya Makuratha akageuka na kuwaona wamekaa eneo lile la mapumziko.
Jordan alianza kusogea pale walipo. Lakini kwa bahati mbaya hakumtambua Nisha kwa sababu amempa mgongo.
Mawazo yote ya Jordan yalikuwa kwenye ile kazi muhimu waliyopewa na Agent Corma. Hakutaka kupoteza hata sekunde moja.
Alipomfikia Makuratha, hakuhangaika hata kuangalia ni nani mwingine aliyekuwa amekaa naye, akijua fika kuwa Makuratha ni mtu wa mambo mengi, huenda anapiga soga na mwanachama mwingine wa Nairobi fighters.
"Makuratha, tulikuambia ukae karibu na Object 0 uangalie maendeleo yake, wewe umekuja kukaa huku na unaona fresh tu? Hujali wala nini..." Jordan alifoka kwa sauti ya chini huku akitoa simu ya Corma mfukoni mwake.
"Haya, nitupie hizo picha kwenye hii simu sasa hivi tuzitume kwa wakubwa."
Makuratha alitaka kufungua mdomo kumjibu, lakini Jordan hakumpa nafasi.
"Tuna kazi ngumu na nyeti ya kufanya, ninyi mmekaa hapa mnapiga stori na kuchekacheka k**a masheteni ya bichi..."
Alisema Jordan lakini mara ghafla aliganda.
Hatimaye macho yake yalitua kwenye sura ya yule mtu wa pili aliyekaa na Makuratha.
Miguu ya Jordan ililegea. Mapigo ya moyo yakaongezeka ghafla.
"Nisha?" Jordan aliita jina la mpenzi wake kwa mshangao.
Alijikuta akimtazama Makuratha kwa jicho la lawama, kisha akarudi kumtazama Nisha. Jasho jembamba likiwa karibu kumtoka.
Jordan anajua wazi kuwa Makuratha ana mdomo mchafu, huenda ameshamwaga sumu mbaya kwa Nisha.
"Amekwambia nini huyu?" Jordan aliuliza huku akimnyooshea Makuratha kidole chake.
"Nisha, usimsikilize anachosema huyu mwanamke, akili zake anazijua mwenyewe, hachelewi kupigisha watu shoti kwa maneno yake ya kipuuzi. Sikia chochote alichokwambia siyo cha kweli, usimuamini." Jordan alipayuka bila hata mpangilio, akijaribu kuzima moto ambao hata hakuujua umewaka kwa kiwango gani.
Nisha alisimama taratibu kutoka kwenye kochi. Uso wake ulikuwa umetawaliwa na huzuni iliyochanganyika na hasira.
"Unataka kusemaje Jordan? Siyo kweli kuhusu nini? Kwani kuna nini kibaya kimetokea? kuna nini unakificha Joo?" Nisha aliuliza kwa sauti yenye utulivu wa kutosha.
Jordan alizidi kuchanganyikiwa. Alisogea hatua moja mbele karibu zaidi na Nisha.
"Nisha nisikilize mimi, siyo kweli, huyu anadanganya tu ili tugombane."
" Kwa nini tugombane?"
Aliuliza Nisha kisha akamwangalia Jordan kwa jicho la huruma na dharau. Akageuka na kumtazama Makuratha ambaye alikuwa amekaa kimya huku akitabasamu kwa kejeli.
Nisha alihisi kabisa hapendwi pia kuna mchezo mchafu unaendelea nyuma ya pazia ambao hajui ni nini. Alimfyonza Jordan kwa nguvu, kisha akageuka na kuanza kuondoka bila kusema neno lingine lolote.
Kitendo hicho kilimuumiza Jordan. Alitamani kumkimbilia Nisha na kumzuia, lakini ghafla mkono wa Makuratha ulimk**ata kwa nguvu.
Makuratha alimvuta Jordan nyuma na kumnong'oneza kwa ukali.
"Acha ujinga wewe mwanaume. Umefuata nini hapa, picha au Nisha? Kumbuka tuna kazi ya kufanya na mabosi wanasubiri ripoti."
Maneno hayo yalimzindua Jordan.
Alijikuta njia panda... kazi au mapenzi?
Jordan alijua akiharibu kazi ya jaribio la Serum-Z, uhai wake utakuwa hatarini. Ilibidi akubali maumivu na kuchagua kazi mbele ya penzi lake kwa Nisha.
Nisha aliendelea kutembea kwenye korido ndefu huku machozi yakimlenga. Hatua zake zilikuwa nzito. Alitegemea kuwa Jordan angemfuata, angeshika mkono wake, na kumuomba msamaha au kumuelewesha kwa sauti ya mahaba nini kinaendelea. Hadi anafika mwisho wa korido, hakuna kilichotokea, Nisha aligeuka nyuma. Alichokiona kilimvunja moyo mara mbili zaidi.
Alimuona Jordan na Makuratha wakiingia chumbani kwa pamoja.
" Why! Why! Why! Jordan" Alisema Nisha kwa sauti ya chini, safari hii akishindwa kabisa kuyadhibiti machozi yasimtoke. Binti wa Meya alilia.
***********
NDANI YA CHUMBA CHA MAKURATHA
Jordan na Makuratha walipoingia ndani na kufunga mlango, walipokelewa na hali ya hewa ya tofauti kabisa.
Walipigwa na harufu kali ya uvundo, iliyofanana na mchanganyiko wa kemikali na nyama iliyoanza kuoza.
"Hii harufu imetoka wapi Makuratha?" Jordan aliuliza huku akiziba pua kwa mkono wake.
Macho yao yalienda kitandani. Yule mlinzi alikuwa bado amelala, lakini mkoromo wake ulikuwa umebadilika. Haikuwa sauti ya mtu aliyelala, bali ilikuwa ni sauti nzito, ya kukwaruza, k**a mnyama anayeunguruma."Alikuwa anaunguruma hivi tangu mwanzo?"
"Mmh hamna alikuwa melala tu kawaida..."
"Umeona sasa haya ndio mabadiliko wazungu wanaka kuona. Hebu tupige picha zingine haraka" Alisema Jordan.
Haraka walimsogelea mlinzi huyo na kumfunua shuka.
Kitu walichokiona katika ngozi ya mlinzi kilikuwa cha kutisha. Mishipa yake ya damu ilikuwa imebadilika rangi na kuwa myeusi tii, ikijichora mwilini mwake k**a ramani. Ngozi yake ilikuwa imepauka.
Jordan hakutaka kuangalia mara mbili. Alipiga picha kadhaa, kisha akazituma zote kwa Bluetooth kwenda kwenye simu ya Agent Corma.
"Baki unamuangalia, nakuja mara moja, napeleka simu kwa Corma ili azirushe Marekani. Usitoke humu ndani" Jordan alitoa maelekezo na kutoka nje akimuacha Makuratha peke yake.
Makuratha alibaki amesimama katikati ya chumba.
Moyo wake ulikuwa ukidunda kwa kasi. Ile harufu na ule mkoromo wa mlinzi vilianza kumtia hofu.
Aliona ni bora aufunge mlango kwa ndani ili mtu mwingine asiingie na kuona maajabu yanayoendelea ndani.
"Yani wazungu jamani, ukute hivi ndivyo wanatengenezaga yale mazombi sijui. Mambo gani haya sasa" Makuratha alilalamika.
Alitembea hadi mlangoni, akashika kitasa na kuanza kunyonga funguo.
Akiwa bado ameshika mlango, ghafla alihisi kitu cha baridi kimemgusa bega lake kulia.
Ilikuwa ni mkono. Mkono mzito, mpana uliokak**aa.
Makuratha aligeuka taratibu, huku akitetemeka kwa hofu kubwa.
ITAENDELEA....
Soma season 4 &5 zote kwa sh 1500/=
Nicheki 0756862047