27/01/2023
SIMULIZI FUPI: PATASHIKA NAFSINI
MWANDISHI: KELVIN CHITANDA
MAWASILIANO: 0629387308
"Hapana bosi sio k**a nimefeli hapana ila."
"Ila nini wewe huna lolote, nilifanya makosa sana kukuamini na laiti ningejua nisingejisumbua"
Mimi ndiye niliyekuwa bosi wake. Nilimkazia macho, sura nikakunja nikauvaa ubosi haswaa. Kwa wakati huo nilijifanya kutopenda longolongo. Chitanda mimi sikuwa Chitanda yule mliyekuwa mmemzoea. Sikuwa Chitanda niliyekuwa nagalagazwa na mpenzi wangu Senorita. Moyo ulinishangaa, nafsi ikanisuta. Kikasalia kicheko tu, kicheko cha chini chini baada ya Beatus kuondoka zake.
Mezani nilisalia mwenyewe. Kikombe cha kahawa mezani. Kiko mdomoni, pembeni yangu kulikuwa na kiti kitupu. Hakikuwa na mtu, ni ambacho alikalia Beatus. Mezani kulikuwa na karatasi nyeupe peeee. Ilikuwa na michoro isiyo na kifani. Ni michoro niliyokuwa naichora mwenyewe nilipokuwa namkaripia Beatus. Yaani nilifanya k**a wafanyavyo waalimu wanapomkaririsha mwanafunzi wafundishapo wanafunzi kadhaa kwenye meza kwa kikoloni inaitwa table teaching.
Nilichukua kikombe kilichokuwa kimetulizana mezani. Muda wote kilitulia tu bila kuchangia chochote katika maongezi yetu mimi na Beatus. Nilikunywa funda la kwanza nikameza, nikanywa funda la pili nikafanikiwa kumeza. Niliazimia kunywa funda la tatu lakini kabla sijafanya hivyo simu yangu iliita.
'Kriiiiii Kriiiiii Kriiiiii Kriiiiiii' iliita kwa kunguruma tu bila kutoa sauti yoyote. Si kwa milio ya simuni wala kwa wimbo wowote wa msanii. Ni kawaida yangu, ndiyo ni kawaida sana kwa simu yangu kutokuwa na mlio. Ni aidha niweke mngurumo ama iite kimya kimya. Sijui ni mazoea ama!
Sikujali kuhusu mlio. Nilipokea kisha nikasogeza simu sikioni.
"Haloo bosi" sauti ilisikika simuni. Jina hilo nilishalizoea hasa katika mazingira ya Dar es salaam. Sio hilo tu bali yapo mengine niliitwa nayo, tajiri, mheshimiwa, kiongozi, papaa, chief, na mengine mengi ya karma hiyo. Hata jina langu la Chitanda lilianza kufifia. Jina ambalo nililipenda sana, nilikuwa na lengo la kulifanya jina hilo kuwa miongoni mwa majina yatakayozungumziwa nchini.
"Naaam naongea na nani?" Niliitika nikaongeza na swali kwa juu.
"Unaongea na Inspekta Odalicus Sixbert, afsa usalama Taifa"
"Mmh kulikoni?"
"Usijali Mr. Chitanda kwa muda mrefu tumefahamu k**a wewe ni jamabazi sugu hapa jijini, jijini Dar es salaaam"
"Mmh jambazi?" Niliuliza kwa mshangao k**a vile nilikiwa sifahamu chochote. Mshangao wangu haukufanya sauti ya simuni kusitisha maongezi. Aliendelea kuongea.
"Eeh ila kwa vile mtandao wako ni mkubwa tumekiri hatukuwezi kwa lolote. Maana mara uonekane hauna hatia mara tushindwe kukuk**ata kabisa, mara tushindwe pa kuanzia. Mimi k**a afsa usalama Taifa nilipenda nikuombe utusaidie kitu"
"Mmh kipi hicho?" Niliuliza swali lingine. Nilikuwa tayari nimeshakubali kuitwa jambazi ingawa sikuwa na wasiwasi wowote. Nilijua mbinu za kutumia endapo k**a zilikuwa mbinu tu za kunitia hatiani. Simu ikiwa bado sikioni nilikumbuka kitu. Nilikumbuka kuhusu mkwara niliokuwa nimempiga Beatus baada ya kumhisi kuvujisha siri. Nilihisi labda alinizunguka na kutoa taarifa katika ngazi za usalama ili kusalimisha nafsi yake. Niliwaza hivyo kwani yeye tu ndiye niliyekuwa nimemdokeza kuhusu tukio la wizi lililokuwa linafuatia.
"Eeh tunaomba uisaidie serikali kuhusu kile kinachoendelea Kibiti!" sauti simuni iliongea hayo ikatulia kusubiri jibu langu.
"Mmh niisaidie serikali? Sasa serikali na mimi nani mwenye nguvu? Au mnataka kuniingiza mtegoni?"
"No...no..no sio hivyo Mr. Chitanda"
"Oh ok endelea, ni kwa namna gani nitaisaidia serikali?"
"Tunataka uwe mpelelezi pale Kibiti kuhusu mauaji yanayoendelea. Tunajua wewe ndiye mtu sahihi utakayekuja na solution ya hili tatizo. Lakini pia utatusaidia kuwafahamu wanaofanya mauaji haya kwasababu wewe una mtandao mkubwa k**a nilivyotangulia kusema hapo awali"
"Sawa, lakini nitawezaje kufanya hivyo?" Niliuliza ingawa sikuwa na hakika k**a angeeleza k**a nilivyokuwa nimemaanisha. Hata hivyo alinielewa swadakta kabisa.
"Usijali kuhusu ulinzi, usijali kuhusu pesa za kuendeshea zoezi. Kuhusu ulinzi utakuwa unashirikiana na jeshi la Kibiti kuanzia jeshi la usalama pamoja na jeshi la polisi. Pesa za uendeshaji utapewa. Lakini pia bila kusahau utataja kiasi utakachokihitaji k**a posho ya zoezi" sauti ilisikika ikatua vema kwenye ngoma ya sikio langu la kushoto. Ilisikika ikakoma kisha kimya kikafuata. Bila shaka niliyekuwa nasubiriwa kusema neno nilikuwa mimi.
Baada ya kufikiri kidogo nilimeza funda la mate nikawa tayari kuongea chochote.
"Inspekta" nilianza kwa kuita.
"Naam bosi" inspekta aliitika akarudia tena kuniita bosi.
"Milioni mia tatu taslimu"
"Hamna shida bosi, naomba kesho Jumatano tukutane nje ya benki ya NMB, Kibiti"
"Benki? Pesa yangu itumwe kwenye akaunti namba yangu masaa manne kabla ya kazi kuanza. Kwahiyo namaanaisha kesho kabla ya saa moja pesa yangu niipate"
“Sawa bosi nipe dakika tano”
“Ok sawa!” nilikubaliana naye nikakata simu.
Ya kwanza, ya pili, ya tatu, ya nne ni dakika hizo. Simu yangu ilikuwa makini sana kuzihesabu. Ilihesabu kwa maringo ya hali ya juu. Moyo nao haukuwa nyuma, uliongeza mapigo ikawa mara mbili yake. Kuna nafsi iliyokuwa inanisuta na kuniambia nisichukulie kawaida.
‘No free lunch in America’ nafsi ilizidi kunisulubu. Moyo nao haukuacha kukoma. Ulizidisha mapigo ikawa kero. Kuna wakati nilitamani nizime simu lakini nikasema hapana ngoja nione itakuwaje yaani ‘liwalo na liwe’.
‘Twiririii’ mngurumo wa kuingia ujumbe simuni mwangu ulisikika. Hapo mapigo ya moyo yalirejea upya, yaliongezeka kasi yake. Haja kubwa ilikuwa inasukuma nguo yangu ya ndani, haja ndogo nayo ilikuwa mbioni kuchomoza.
‘Ila hawa sio k**a wanataka kuniweka mikononi mwao? Serikali ishirikiane na jambazi? —Jambazi sugu. Mimi hii nahisi ni danganya toto tu, nisipoangalia naweza kuozea jela kirahisi sana’ niliwaza huku nikifanya zoezi la kufungua ujumbe uliokuwa umeingia simuni mwangu.
Licha ya kutandwa na wasiwasi pima niliomba ujumbe uliongia uwe wa pesa k**a nilivyokuwa nimefikiri. Nilifanikiwa kufungua ujumbe ukasomeka hivi;
“Ndugu mteja wa NMB Umepokea kiasi cha shilingi 300, 000,000.00 kwenye akaunti yako inayoishia na 5020. Tembelea Benki ya NMB au wakala aliye karibu yako ili uweze kutoa kiasi chochote cha pesa. NMB karibu yako!” ujumbe ukakoma.
‘Mmh ujambazi sasa basi, kupanda daladala basi tena. Nitawamisi niliokuwa nafanya nao kazi k**a akina Beatus—kwa sasa mimi siyo wa karma yao tena. Kwa sasa mimi si’ wakuangalia mpira kwenye vibanda umiza tena, si’ wa kunywa juisi za miwa zilizotengenezwa bila viwango. Hata hivyo naomba tu niwakumbuke wazazi wangu ili nipate baraka zao hata ikifika hatua ya mwenyezi kuwanyakua.’
Niliinuka nilipokuwa nimekaa kisha kwa furaha nikaanza kurukaruka huku nipiga kelele za ushindi. Lo! Nishtuka baada ya kushtuliwa na aliyekuwa ameketi kwa pembeni yangu. Alikuwa mdada aliyekuwa ameupamba vema uso wake. Vishimo vidogo kwenye mashavu yake na macho legelege aliyokuwa nayo viliupamba uso wake.
“Mmh kwani nipo wapi?” niliuliza kwa mshangao mkubwa sana.
“Upo kwenye daladala ya Makumbusho kwani vipi?”
“Ndoto”
“Ndoto? Imefanyeje tena? Maana me nimeambulia kusikia ukisema ‘kupanda daladala sasa basi nikahisi labda kuna lolote umeliona humu garini. Labda kuna aliyeingia na misukule. Imekuaje kaka?” Alinidokeza akanitandika swali bila huruma. Angejua!
“Hapaa usijali nilikuwa ndotoni tu. Lakini ni ndoto ya kawaida tu. Hamna lolote baya”
Nilijihisi aibu sana kwa yale yaliyokuwa yamenitokea mbele ya mrembo ambaye alichukua umakini wake wote kuniuliza kilichonitokea. Sikumsimulia nilichoota nikamwacha abaki na maswali kichwani. Safari iliendelea ingawa sikuwa na hamu ya kulala tena. Mkononi nilishika kitabu cha SAFARI YA MAPITO nilichokuwa nakipeleka kwa mteja aliyekuwa amenielekeza anapopatikana na anuani yake—Makumbusho.
‘Mmh ndoto zingine bwana sijui zina maana gani?’ niliwaza nafsini. Sikuwa na jibu la moja kwa moja ingawa nilikumbuka kilichonifanya nipitiwe na usingizi—Madeni. Madeni yalinizonga kitu ambacho yalikuwa yananifikirisha kila wakati.
‘Kwanini ile ndoto isingekuwa ya kweli tu’ niliongeza kuwaza. Hata hivyo isingewezekana hata kidogo kwani siku zote maji hayapandi mlima. Kwahiyo kuhusu milioni mia tatu zilibaki kuwa za kwenye ndoto tu tena ndoto ya mchana.
MWISHO
PATA NAKALA YA KITABU CHA SAFARI YA MAPITO KWA BEI YA SHILINGI ELFU KUMI TU. MIKOANI TUNATUMA, KWA WALIO DAR UNALETEWA. WASILIANA NASI KWA NAMBARI 0629387308.
Kelvin Chitanda,
Dar es salaam, Tanzania.