21/03/2024
DAR ES SALAAM;
Mhashamu JUDE THADDEUS RUWA'ICHI, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la DAR ES SALAAM ametoa wito kwa Wakristo wakatoliki na wananchi wote kushiriki mbio za riadha zinazoandaliwa na Jimbo, ili kuwasaidia wahitaji, kuboresha kituo cha hija PUGU na Maktaba ya MWL. NYERERE.
Askofu Mkuu RUWA’ICHI amesema hayo leo Machi 21, 2024 wakati akizindua rasmi maandalizi ya awamu ya pili ya mbio hizo za riadha maarufu k**a PUGU MARATHON 2024 zinazotarajiwa kufanyika Mei 18, 2024 kuanzia saa 12 asubuhi katika viwanja vya kituo cha hija cha PUGU jijini DAR ES SALAAM.
Akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa mikutano Kanisa Kuu la Mtakatifu YOSEFU jijini DAR ES SALAAM, Askofu Mkuu RUWA’ICHI amesema gharama ya kujisajili ni shilingi elfu 30, na kwamba kutakuwa matembezi na riadha ya umbali tofauti kadri ya uwezo wa mshiriki.
Aidha ameongeza kuwa, katika mbio za mwaka jana walifanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi milioni 117 na laki 5, ambacho kilitumika kununua mashuka 50 kwa ajili ya Hospitali ya Kardinali RUGAMBWA, kulipa ada ya watoto wasio na uwezo, kuweka umeme katika nyumba iliyotumiwa na Hayati Baba wa Taifa, MWL. NYERERE alipokuwa akifundisha PUGU pamoja na maboresho ya kituo cha hija.
Naye Meneja wa Kidigitali kutoka Benki ya MKOMBOZI, FILEMON TESHA akielezea namna ya kujisajili amesema, usajili unafanyika kupitia simu ya mkononi, mawakala wa benki hiyo na katika matawi yao yote nchini.