17/04/2026
Kuandika ni jambo moja, kujua kundika ni jambo mbali. K**a ilivyo kusoma na kujua maana ya kile ulichosoma.
Lugha ni chombo cha mawasiliano; tunawasiliana kwa kutumia ishara, sauti, maandishi kwa njia nyingi na mbinu mutawalia.
Bahati imenifanya kuwa mwandishi - mwandishi wa vitabu. Kwa ushairi na mjazo.
Bahati hiyo hiyo imenikutanisha na watu wenye kustahiki umufti katika uandishi; kwa fasaha na akili kubwa waliyonayo.
Watu weledi wanaojua kuchagua maneno wazungumzapo. Wanaojua kudhibiti hisia ukikabiliana nao. Watu walio tayari kujifunza hata herufi moja yenye manufaa kwao binafsi na tasnia ya uandishi wa vitabu katika ujumla wake.
Tasnia ya vitabu tangu zamani imekumbwa na nak**a za choyo, hasad na ulafi kutoka kwa wanaosimamia uchapaji na usambazaji.
Pengine tunaweza kuwaita wanaoshikilia nguzo ya uandishi wa vitabu.
Ukelele wa mabadiliko umekuwepo tangu enzi za kina Saadan Abdu Kandoro, Shafi Adam Shafi na waandishi wa zama hizi.
Hofu imepumbaza mapambano haya; yakakosa mnyororo wa mwendelezo kutoka kizazi kimoja kwenda cha pili.
Huibuka tu kundi likalalamika, likahanikiza mabadiliko kisha likafa kifo cha asili.
Ni k**a majilio ya radi yanyakuavyo usikivu wa mwanadamu kwa ghafula. Kisha kukapiga kimya.
Mimi na wenzangu tunataka kuukata mduara huu wa utesi na unyonge.
Tumeanza kwa kukutana kujadili chanzo cha matatizo yetu. Kwa sababu mwenye akili za desturi hutazama alipojikwaa si alipoangukia.
Kwa kutaniko letu la kwanza lililofanyika Dar es Salaam, Aprili 12, 2026. Tumejadili mengi.
Jumla ya tuliyojadili ni mamna gani tutazitumia akili, kalamu na sauti zetu kuukabili huu utesi.
Ni mtu mjinga tu ataacha kufanya hiki tunachokifanya kwa mustakabali wa fani nzima ya uandishi wa vitabu.
Hatutaki baada ya miaka 100 ijayo wajukuu zetu waone aibu kutaja majina yetu kwenye meza za majadiliano, kuwa babu zao tulipata kuwa waandishi wa vitabu; kwa sababu tu majina yetu yatakuwa katika orodha ya watu waoga.
*** Imeandikwa na Hafidh Kido