Soma Kiswahili

Soma Kiswahili Kwa utunzi wa shairi au jambo lolote kuhusu Kiswahili tafadhali wasiliana na +255787280042

Huu ni ukurasa mahususi unaowasaidia watu Duniani kujifunza lugha ya Kiswahili kwa kutumia mbinu rahisi na za kiushawishi

23/08/2025

Ushairi Ni Kazi ya Moyo, Fikra na Taaluma.

Na Mkuluwanyika.

Ushairi wa Kiswahili si kazi rahisi na ya kawaida wala si jambo linalotendeka papo kwa papo. Kuunda shairi la Kiswahili lenye mvuto na ubora ni mchakato mrefu unaohitaji utaalamu, hekima na ubunifu wa hali ya juu. Si kazi ya hatua moja tu, bali ni safari ndefu ya ubunifu inayoanzia ndani ya nafsi ya mshairi.
Mchakato wa Ubunifu wa Ushairi
Kutunga shairi awali huanzia na hatua ya kutafuta wazo. Wazo litakaloibuliwa na mshairi laweza kuwa dogo na la kawaida, lakini humlazimu mshairi alichunguze kwa kina, alipime na alichimbue haswaa hadi apate kiini chake chenye utoshelevu wa hakika isiyo na punje ya shaka ndani yake.

Hatua inayofuatia huwa ni kuchagua muundo wa shairi; je, mshairi atatumia aina gani ya shairi? Hapa ndipo mshairi anapoanza kujikuta kwenye changamoto kubwa ya kuzingatia sheria na kaida za ushairi wa Kiswahili. Hizi ni pamoja na uwepo wa vina, mizani , beti na mishororo . Hapa ndipo ugumu unapoanzia kwani inamlazimu mshairi afikirie namna ya kuupanga ujumbe wake ili ufikishwe kikamilifu huku akizingatia sheria zinazoendana na muundo husika,sheria ambazo kwa namna yoyote ile zinahitaji ufundi wa hali ya juu kuzitimiza.
Mshairi huwa hanabudi kuzitambua kaida za miundo ya mashairi ,ili iwe rahisi kuchagua muundo unaoendana na aina ya wazo alilonalo,mfano ikiwa ana wazo la kuandika shairi la wasifu itamlazimu atambue kanuni na taratibu za kuandika utenzi na itakuwa hivyo kwa aina nyingine yoyote ya muundo atakaoutumia ikiwa ni tarbia, ngonjera, ukawafi, kikwamba, zingo, kisarambe na miundo mingineyo. Ulazima huo ni k**a ule wa fundi mwashi anapokabidhiwa ramani ya jengo na eneo la kujenga, humpasa kufahamu je ramani hiyo alonayo yaendana na eneo husika na je jengo atakalojenga litakuwa katika taswira iliyokusudiwa na inayohitajika?

Jambo la Tatu: Mtindo wa Shairi
Mtindo wa shairi unahusu jinsi mshairi anavyowasilisha wazo au ujumbe wake. Hapa kunajumuisha uchaguzi wa maneno, matumizi ya tamathali za semi, na jinsi lugha inavyotumiwa kuunda hisia fulani. Kwa kuwa USHAIRI ni sanaa inayozingatia arudhi nasi lugh ya nathari,mshairi bora anahitaji matumizi umbuji zaidi wa kufahamu lugha na usahihi wa matumizi ya lugha katika shairi. Katika mtindo mshairi anatakiwa kuwa mbunifu na kuhusisha matumizi ya:
* Tanakali za Sauti: Mbinu ya kutumia maneno yanayoiga sauti au hali fulani, au namna kitendo kilivyofanyika.
* Tashbihi: Mbinu ya lugha inayolinganisha vitu au hali mbili tofauti kwa kutumia maneno ya kulinganisha, k**a 'k**a', 'mithili ya', 'sawa na', au 'ja'.
* Istiara/Sitiari: Mbinu ya kulinganisha vitu viwili moja kwa moja bila kutumia viunganishi.
* Jazanda: Kitu au mtu huwakilishwa na kitu kingine kinachofanana naye kwa sifa au tabia. Tofauti na tashbihi, jazanda haitumii maneno ya kulinganisha. Mfano: "Yule mama ni simba."
* Taashira: Matumizi ya lugha ya ishara kuwakilisha ujumbe fulani. Jina au kitu fulani kinatumika kumaanisha kitu kingine chenye uhusiano na kile kilichotumiwa.
* Taswira: Matumizi ya lugha/maneno yanayojenga picha ya hali au jambo fulani kwa msomaji.
* Tashihisi: Mbinu ya kupatia kitu kisicho na uhai sifa za kiumbe mwenye uhai (sifa za kibinadamu). Huu huitwa uhuishaji.
* Chuku: Kutumia maneno yaliyotiliwa chumvi ili kusisitiza ujumbe fulani au kusifia kitu.
* Takriri: Mbinu ya kurudiarudia neno moja au kifungu cha maneno ili kusisitiza ujumbe fulani.
* Tanakuzi: Mbinu ya kusisitiza ujumbe kwa kuambatanisha maneno ya kinyume au yanayokinzana.
* Majazi: Ni ufundi wa lugha ambapo mshairi hutumia majina, majina ya mahali, au majina ya vitu vyenye maana ya ndani au siri.
* Lakabu: Mbinu ya mhusika kupewa au kubandikwa jina na wahusika wengine, ama yeye mwenyewe.
* Semi: Fungu la maneno linapotumika kutoa maana nyingine, badala ya ile ya maneno yaliyotumika. Semi hutumika kuficha ukali wa maneno au kupamba lugha. Kuna aina mbili za semi:
* Nahau: Huwa na vitenzi.
* Misemo: Haina vitenzi.
* Methali: Ni misemo ya hekima yenye maana iliyofumbwa.
* Maswali ya Balagha: Ni maswali yanayoulizwa kutumia tamathali za semi, methali, nahau na hata vitendawili ili kuongeza ladha na undani wa shairi.

Kwakuwa kazi ya mshairi ni kujenga picha katika akili za wasikilizaji na wasomaji, na hili linawezekana tu kupitia matumizi ya hayo mambo yaliyotajwa.

Utoshelezi na Muwala
Safari ya mshairi haiishii katika muundo na mtindo pekee. Ili kulifanya shairi lake liwe bora,mshairi atahitajia utoshelezi na muwala ili ujumbe wake uwe mzito na wenye maana ya kina.
* Utoshelezi: Katika shairi la Kiswahili, maana yake ni hali ya kila ubeti kujitosheleza kwa habari au ujumbe unaompa msomaji ili afahamu maelezo ya ubeti huo kikamilifu. Hii inaendelea kwa mtiririko unaoeleweka kutoka ubeti mmoja hadi mwingine.
* Muwala: Ni mtiririko wa fani na mawazo ulio na mantiki katika shairi. Katika taaluma ya ushairi, kuna aina mbili za muwala:
* Mawazo ya ubeti yanapaswa kufuatana kwa ufasaha kutoka fatahi, mroto, mleo, na kituo ili kuyajenga mawazo kikamilifu.
* Sheria ya pili ni muwala wa beti lazima uwe na mtiririko mzuri wa mawazo kutoka ubeti hadi ubeti. Katika aina hii, mawazo huwa yamefungamana na maudhui ya tungo na huwa yamekamilika.
Hapa, unapochambua kwa kina, utaona ugumu wa utunzi wa shairi. Sio jambo jepesi kwa mshairi kuhakikisha anakamilisha hali ya utoshelezi katika kila ubeti, yaani aeleze jambo lenye maana, lakini wakati huo huo maana hiyo isigongane na maana ya beti nyingine na ilete mtiririko unaoeleweka katika muktadha wa maudhui mama. Mfano, ubeti wa utangulizi wa shairi hauwezi kuwa katikati ya utungo na ubeti wa kaditama hautakiwi kuwa katika mukadima.

Sio Kila Mwandishi ni Mshairi
Kwa ugumu na ukweli kwamba ushairi si kitu rahisi, ndipo ikawa si kila mwandishi ni mshairi.
Waswahili wanasema, "Mashairi bora si ya mtu wa kawaida." Kwa hakika, si kila mtu anaweza kuwa mshairi. Inahitaji hekima na utambuzi wa lugha ya hali ya juu. Washairi ni watu wachache waliopatiwa karama ya kuunda maneno ambayo thamani yake ni kubwa sana. Huenda ndiyo maana kuna usemi usemao, "Ukiondoa vitabu vitukufu vya dini ambavyo vinaweza kuongoa imani, matendo na fikra za watu, vinavyofuata ni vitabu vya ushairi."
Ikiwa mtu anaweza kuyafinya maneno machache kwa mipaka ya sheria na kanuni na yakaleta maana pana, basi ni hakika hawezi kushindwa kuelezea mambo kwa kutumia maneno marefu pasipo kubanwa na sheria ngumu mahsusi. Ndipo ikawa mtu anayeweza kuandika shairi anaweza kuandika kitu chochote nje ya ushairi kwa ufasaha na ubora wa hali ya juu. Ni washairi pekee ambao hutumia taaluma yao ya lugha kufinyanga maneno na kuunda kazi za sanaa ambazo hufikia hisia za binadamu kwa namna ya kipekee,huo ndio msingi wa ithibati ya kuwa kila mshairi ni mwandishi, lakini si kila mwandishi anaweza kuwa mshairi kwa ubora wa kishairi.

Tuuthamini na Kuulinda Ushairi Wetu
Tusiuache ushairi wetu wa Kiswahili upotee. Tusiudharau ushairi wala kuwadharau washairi. Ni jukumu letu kuulinda, kuuthamini, na kuutukuza, kwani ni hazina ya fikra na chemchemi ya lugha yetu. Tutambue mashairi yanatukumbusha kuhusu historia yetu, utamaduni wetu, na maadili yetu. Tuwathamini washairi kwa kutambua athari na mchango wao katika jamii. Ama kwa hakika washairi huacha alama isiyofutika katika historia ya lugha yetu.
Binafsi, sitoyasahau matukio matatu ambayo nayahesabu k**a alama zisizofutika katika sanaa yangu ya ushairi.
Tukio la Kwanza: Niliwahi kuombwa kutunga shairi kuhusu madrasa iliyokuwa katika mazingira magumu. Wanafunzi walisoma barazani, tena katika nyumba ya udongo, na mwalimu wao alitembea umbali mrefu kufundisha bila mshahara wala posho. Nilipoomba kuwasemea, nilitunga shairi na kupaza sauti. Kwa hakika, sauti ilifika mbali na hatimaye madrasa hiyo, kutoka Msambweni, Kenya, imejengwa ya kisasa na mwalimu naye amejengewa sehemu ya kuishi.
Jambo la Pili: Kupitia kero hiyo, nilipaza sauti kuwasemea walimu wa madrasa na hatimaye kukazaliwa UMATA (Umoja wa Maimamu Tanzania). Kupitia umoja huo, semina na makongamano yalifanyika kuendeleza maendeleo ya walimu wa madrasa kiuchumi na kielimu. UMATA ikawa sababu ya taratibu nyingine zenye mlengo wa kutatua kero za walimu wa madrasa kupatikana.
Na Jambo la Tatu: Ni pale nilipochoshwa na kero ya maji iliyokuwa imetamalaki wilayani Ubungo, Dar es Salaam. Nilitunga shairi lenye kuisemea kero hiyo, na shairi likafika hadi kwa wahusika. Hatimaye, kero hiyo ilitatuliwa, na nilishuhudia hilo.
Hivyo, ushairi si fani ya malumbano na majigambo pekee; ni fani yenye kuibua kero na matatizo ya jamii. Ni fani yenye kuunganisha watu na kulinda tamaduni, ni urithi na silaha dhidi ya upotovu wote.
Si mimi tu niliyewahi kuleta athari chanya zenye kunufaisha watu kupitia ushairi. Ni washairi wengi waliopita, waliopo, na wajao, na itabaki hivyo hadi mwisho wa dunia.
Hivyo basi, ushairi uenziwe, ushairi utukuzwe.

SHAIRI: NIKIFA NIZIKWE KWETUShairi hili ni ndia, mauti yakithubutu,Naamba zangu hisia, musije nitupa mwitu,Pangu pakujid...
02/08/2025

SHAIRI: NIKIFA NIZIKWE KWETU

Shairi hili ni ndia, mauti yakithubutu,
Naamba zangu hisia, musije nitupa mwitu,
Pangu pakujidahia, pazuri sio fukutu,
Nikifa nizikwe kwetu wanangu nawahusia.

Hata nifie India, au mji wa Timbuktu,
Fanyeni usalimia, na mutie na waitu,
Rambirambi kuchangia, muuchezavyo upatu,
Nikifa nizikwe kwetu wanangu nawahusia.

Tafuteni baharia, anayepajua kwetu,
Jahazini kunitia, nifike maji kukutu,
Akinishusha Mafia, huo basi ndio utu,
Nikifa nizikwe kwetu wanangu nawahusia.

Ugumu ukiwajia, nitiwe kwenye matatu,
Ndani pamwe abiria, apajuaye baitu,
Isangala, Songwe pia, kuna makaburi yetu,
Nikifa nizikwe kwetu wanangu nawahusia.

Nikoshwe kwenye Dunia, najisi nitoke kutu,
Sanda nikijivalia, isije chafuka katu,
Vyema mukinisalia, k**a agano na watu,
Nikifa nizikwe kwetu wanangu nawahusia.

Kuzikwa kijahilia, nakataa katukatu,
Mimi muisilamia, kinyume sije thubutu,
Masiku yakiwadia, niagwe na lailatu,
Nikifa nizikwe kwetu wanangu nawahusia.

Sitaki wapa udhia, maneno yangu ni butu,
Mapema nawaambia, musije chukia mtu,
Pesa za kunizikia, zipo mlango wa tatu,
Nikifa nizikwe kwetu wanangu nawahusia.

Lakabu: Msafwa Wavisiwani
Malenga: Dadi Ntanila Ally
PoeticHR

TUSOME NA TUULINDE USHAIRI WA KISWAHILI KWA MASLAHI MAPANA YA USHAIRI NA UTAMADUNI WA MSWAHILIAmeandika: Hamis Ally S. K...
23/07/2025

TUSOME NA TUULINDE USHAIRI WA KISWAHILI KWA MASLAHI MAPANA YA USHAIRI NA UTAMADUNI WA MSWAHILI

Ameandika: Hamis Ally S. Kisamvu (Mkanyaji)

Utangulizi

Katika ushairi wa Kiswahili halisi(wakimapokeo), kila aina ya shairi hujipambanua kwa muundo, mizani, na madhumuni.Kuna aina nyingi sana ya mashairi kutokana na miundo yake ikiwemo tarbia, shairi lenye mistari minne kwa kila beti ,na huwa na beti chache sana ili kutilia mkazo ujumbe mfupi unaogonga moyo mara moja (Mulokozi, 1996).

Tarbia ni Nini?

Neno “tarbia” linatokana na neno la Kiarabu رُبَاعِيَّة (rubāʿiyyah), likimaanisha kitu chenye vinne. Katika muktadha wa ushairi wa Kiswahili, tarbia humaanisha shairi lenye mistari minne kwa kila beti, na kawaida huwa na jumla ya beti 3–10 tu (Knappert, 1967). Muundo huu mfupi unasaidia kufikisha wazo, hisia au busara kwa haraka na kwa athari kubwa.

Hata hivyo, kumekuwepo na jaribio la kuandika tarbia ndefu mno, zenye beti 30 hadi 100, jambo linalokiuka utaratibu wa kifasihi na kupotosha dhana ya tarbia.

Kwa Nini Si Sahihi Kuandika Tarbia ya Beti 30–100?

Inapoteza Sura ya Tarbia: Tarbia ndefu hujigeuza kuwa aina nyingine ya shairi k**a kasida au utenzi, hivyo hupoteza utambulisho wake wa kiasili (Harries, 1962).

Athari ya Haraka Hupungua: Lengo la tarbia ni mchomo mfupi wa fikra. Urefu uliokithiri huchosha hadhira na kupunguza makali ya ujumbe (Mazrui & Shariff, 1994).

Kinyume na Mila ya Kihistoria: Watunzi wa jadi k**a Muyaka bin Haji na Amri Abedi hawakuwahi kuandika tarbia ndefu; waliihifadhi kwa tungo fupi zenye ufanisi (Mulokozi, 1996).

Kanuni ya Mtindo na Aina: Ukivunja sifa za msingi — idadi ya beti na urefu — hutakiwi tena kutumia jina “tarbia”; kufanya hivyo ni kosa la kitaaluma (CHAKITA, 2002).

Hitimisho

Kwa mujibu wa ushahidi wa kihistoria na kitaaluma, tarbia inapaswa kubaki na urefu mfupi. Kuandika tarbia yenye beti 30 hadi 100 ni kinyume na misingi ya utanzu huu na humdanganya msomaji kuhusu aina ya kazi anayokabiliana nayo.

Mapendekezo kwa Watunzi

Iwapo ujumbe wako ni mrefu, tumia kasida, utenzi au aina nyingine ndefu. Hakikisha unazingatia vigezo vya kila aina ili kulinda uhalisia wa kazi ya fasihi.

Marejeo (APA 7th Edition)

1. Chama cha Kiswahili cha Afrika Mashariki. (2002). Mwongozo wa Uandishi wa Ushairi. Nairobi, Kenya: CHAKITA Publishers.

2. Harries, L. (1962). Swahili Poetry. Oxford, UK: Clarendon Press.

3. Knappert, J. (1967). Four Centuries of Swahili Verse: A Literary History and Anthology. London, UK: Heinemann.

4. Mazrui, A. A., & Shariff, I. N. (1994). The Swahili: Idiom and Identity of an African People. Trenton, NJ: Africa World Press.

5. Mulokozi, M. M. (1996). Ufundishaji wa Fasihi ya Kiswahili. Dar es Salaam, Tanzania: Dar es Salaam University Press.

6. Nassir, A. (1980). Tungo za Ushairi. Nairobi, Kenya: Heinemann.

*Pichani Mshairi Nguli Almarkhum Sihiyana Swalehe Mandevu.

MUUNDO WA SHAIRI NDIO  TASWIRA YA SHAIRI HUSIKA.Na Mkulu Wanyika.UTANGULIZINimesoma makala yenye anuani isemayo “Dhana y...
23/07/2025

MUUNDO WA SHAIRI NDIO TASWIRA YA SHAIRI HUSIKA.

Na Mkulu Wanyika.

UTANGULIZI

Nimesoma makala yenye anuani isemayo “Dhana ya Ufupi na Urefu Katika Shairi la Kiswahili” iliyotungwa na mtu nisiyemfahamu katika ulimwengu wa ushairi. Ni mada yenye mchango wa kifasihi unaokusudia kutetea mtazamo wa kuruhusu utunzi wa mashairi ya Kiswahili yenye beti nyingi bila kuzingatia mipaka ya muundo wa shairi.

Awali yafaa ieleweke kuna ushairi na shairi .
Ushairi ni sanaa ya lugha inayotumia mpangilio maalumu wa maneno, vina, mizani, na hisia ili kueleza mawazo, hisia, maadili au falsafa kwa njia ya kipekee, na yenye mvuto wa kifasihi. Ushairi unaweza kuwasilishwa kwa njia ya mdomo au maandishi, na mara nyingi hutegemea matumizi ya lugha ya picha, tamathali za semi, taswira, na muundo maalum wa kishairi.
(Mulokozi, M. A. B. – Fasihi ya Kiswahili: Nadharia na Historia)

Ushairi k**a fani zingine una misingi yake.
Wanazuoni wa Kiswahili wamebainisha misingi hiyo ikiwa ni sifa kuu zinazotofautisha ushairi na aina nyingine za fasihi andishi, ambayo ni:

1. Utaratibu wa vina na mizani
Maneno katika beti huwekewa vina na idadi maalum ya mizani au silabi kwa kila mstari.

2. Lugha ya mkato na ishara
Ushairi hutumia lugha fupi, ya kuvuta fikra, na yenye maumbo ya kifasihi – sio ya moja kwa moja (nathari).

3. Hisia na uzito wa ujumbe
Mashairi hubeba hisia nzito k**a huzuni, furaha, ghadhabu, mapenzi, au mshik**ano wa kijamii na kidini.

4. Muundo maalum
Ushairi ni sanaa ambayo ina miundo yake.
“Muundo wa shairi ni mpangilio wa nje wa shairi unaohusisha idadi ya mistari kwa kila ubeti, vina, mizani, radifu, na kibwagizo.”
(Chimera, 2000: 201–205)

Kwa kuwa muundo huonesha umbo la nje la fasihi, hapo ndipo tunapopata aina tofauti za mashairi (bahari).
Aina ambayo tunaizungumzia katika mukhtadha wa mada husika ni shairi, na sitoenda mbali kuelezea maana ya shairi na rejea nukuu ileile iliyoletwa katika makala ya “Dhana ya Ufupi na Urefu Katika Shairi la Kiswahili”.

Shairi ni nini?
Njogu na Chimerah (1999:100) wanafasili kuwa shairi ni utungo wenye mishororo minne au zaidi kwa kila ubeti. Wakaendelea kueleza kuwa utungo huo ukiwa na mishororo minne unaitwa tarbia na mitano ni takhmisa. Pia, King'ei na Kemoli (2001:18) wanasema kuwa shairi ni utungo wenye mishororo minne katika beti zake. Kidesturi, shairi huwa na mishororo iliyogawika katika vipande viwili-viwili. Kila kipande huwa na mizani nane. Shairi huwa na vina vya kati na vya mwisho na aghalabu vina vya ndani na vya nje; vilevile huwa na urari. Wakati mwingine, mshororo wa mwisho (kibwagizo) huwa na utaratibu wa kuteua vina vinavyotofautiana na vina katika mishororo tangulizi.

Kwa upande wake, Wamitila (2003:191) anasema shairi ni utungo ambao una mistari iliyogawika katika mafungu kadha.
Naye, Nabhany (2006:4) anaeleza shairi ni bahari ya ushairi ambayo huwa na mishororo minne. Vina vya kati hulingana na vya mwisho kadhalika, lakini mshororo wa mwisho kina cha mwisho huweza kuja kati na cha kati kikaja mwisho. Kwa jumla, fasili hizo zinatuangazia mambo yafuatayo:

Shairi ni utungo wa kishairi;

Shairi ni mojawapo ya bahari ya ushairi;

Aghalabu shairi huwa na mishororo minne iliyogawika kwenye vipande viwili; likiwa na mishororo minne huitwa tarbia;

Shairi lina vina vya kati na mwisho; na

Shairi lina kibwagizo.

Kwa sifa zilizotajwa katika muundo huo wa shairi, hapana shaka aina ya shairi lililotajwa hapo kwa kawaida ni shairi la tarbia .

Nahapo ndipo tunafika katika kiini cha mada yetu: Je, tarbia ni muundo wa kuandikia mashairi marefu?

Profesa Said Ahmed Khamis (2000:102) katika kazi yake Ushairi wa Kiswahili: Nadharia na Misingi anaelezea kinaga ubaga kuhusu tarbia:

“Tarbia, k**a bahari ya kishairi, imeumbwa kwa ajili ya fikra fupi zenye nguvu, aghalabu za kihisia, falsafa au tahadhari. Mshairi anayepanua tarbia hadi kuwa na beti zaidi ya hamsini hujilazimisha kuleta muundo usio na nafasi ya kina katika uendelevu wa simulizi.”

Siyeye tu hata Mulokozi (1996:34) katika Theory and Practice of Swahili Poetry anasema:
“Mashairi ya Kiswahili ya mapokeo hayakuwahi kuwa na beti nyingi kwa mtindo wa tarbia. Ikiwa kazi ilikuwa ya simulizi au ndefu, basi ilibebwa na utendi au tenzi.”

Kwa minajili hiyo tunabaini ya kwamba kutokana na muundo wake, tarbia haikubuniwa kwa ajili ya mashairi marefu au simulizi ndefu. Mwandishi anapochagua tarbia kuandika shairi la beti mia, anatenda kosa la kiuundaji kwani huziba uwezo wa shairi kuwa na mpangilio wenye pumziko la kimuktadha.

Je, mshairi mwenye mawazo marefu na anahitaji kuyawasilisha afanyaje?
K**a tulivyoona kuwa kila shairi lina muundo wake na muundo ndio hutofautisha aina ya shairi, aina rasmi iliyoteuliwa kwa ajili ya shairi refu ni tenzi. Mshairi anayehitaji kuwasilisha mawazo yake marefu au masimulizi hakatazwi kufanya hivyo, ila aandike katika mtindo wa tenzi.

Abdulaziz, M. H. (1979:87) katika The History of Swahili Prosody anasema:

“Tenzi, kwa asili na maumbile yake, ni aina ya shairi lililobuniwa kubeba kazi za muda mrefu, simulizi, vita, mafunzo ya kidini au historia. Kazi hizi huweza kuwa na beti zaidi ya mia moja hadi mia tatu, jambo ambalo haliwezekani kwa tarbia.”

Kazi za kishairi za kale k**a Utendi wa Inkishafi wenye beti 112, na Utendi wa Tambuka wenye zaidi ya beti 1000 ni mifano hai ya mashairi marefu yaliyoandikwa katika muundo wa tenzi, si tarbia.
Hata Shaban Robert (1954) katika Diwani ya Utenzi wa Vita vya Uhuru alitumia tenzi kutekeleza kazi yake ndefu ya kihistoria badala ya tarbia, akielewa kuwa kuna mipaka ya kimuundo katika shairi la tarbia.

Aidha, Mazrui na Shariff (1994:93) katika The Swahili: Idiom and Identity of an African People wanabainisha kuwa:

“Tenzi ndizo zilitumika katika kazi za kihistoria au simulizi ndefu k**a Utendi wa Tambuka, Utendi wa Mwana Kupona, kwa sababu ya uwezo wa kimuundo wa kubeba mkondo mrefu wa simulizi kwa vina mabadiliko na taratibu pana zaidi ya tarbia.”

Mtunzi anapotaka kuandika kazi yenye beti 100 au zaidi, anapaswa kubadilisha bahari ya shairi, si kulazimisha tarbia kubeba mzigo ambao haukubuniwa kubeba. Hili linaendana na kauli ya Mulokozi (2000:27):

“Bahari huchaguliwa kwa mujibu wa dhima ya shairi; si shairi kulazimishwa kwa bahari.”

Katika makala niliyosoma, mwandishi amewataja washairi k**a Shaaban Robert, Nassir Bhalo, na Akilimali waliotunga mashairi ya beti 30-40 ili kuhalalisha shairi refu hata likiwa na beti zaidi ya mia . Lakini mfano huu si sahihi kwa kuwa hakuna aliyewahi kutumia tarbia kuandika shairi la beti zaidi ya hamsini kwa mtindo wa mapokeo, na ikitokea mtu akafanya hivyo kwa kujua au kutokujua, yatahesabiwa ni makosa k**a makosa mengine yanayotendeka katika kazi za fasihi bila kuangalia hadhi, jina wala wadhifa wake.
Hasa ikizingatiwa hakuna rejea halisi kwa wanamapokeo ya kuhalalisha hilo.
Anayetaka kuhalalisha kazi ya beti mia kwa tarbia, basi aonyesha mfano wa Malenga waliotunga hivyo.

Mazrui (1975) katika The Swahili Poetic Tradition anasema:

“Urefu wa shairi si jambo la hiari pekee, bali ni sehemu ya maumbile ya aina ya shairi. Aina k**a tarbia hutaka msisitizo na ufinyu; tenzi ni k**a mto unaobeba mengi kwa utaratibu mpana.”

Yafaa ifahamike vizuri ya kuwa urefu wa mashairi si suala la dhamira peke, bali pia ni suala la muundo.

Wamitila (2003:191) amesisitiza hilo aliposema:

“Bahari ya shairi ni k**a kiunzi cha sanaa ya mjengo: haipaswi kuvunjwa ovyo kwa madai ya ubunifu. Mshairi anapojifunza kujifunga, hapo ndipo hubuni kwa kiwango cha juu.”

Kutoa hoja kuwa mtu anaweza kuandika chochote kwa muundo wowote ni kuharibu misingi ya ushairi wa Kiswahili wa kimapokeo. Mshairi halisi hujifunza mipaka ya bahari ili afungue milango ya ubunifu wake ndani ya ukomo huo. Hakuna uhuru usio mipaka.

Mwisho, niendelee kuwakumbusha washairi ambao wanaleta upotoshaji pengine kutokana na sababu zao binafsi zinazowasukumia katika ushabiki ama kwa kutafuta umaarufu:
Tarbia haipaswi kutumika kuandika mashairi ya beti ndefu, kwani haikuundwa kwa ajili hiyo.

Tenzi ndio bahari sahihi kwa kazi ndefu, za simulizi, historia au mafunzo ya kina kupitia ushairi,kwenye tenzi unaruhusiwa hata beti zaidi ya elfu .

Malenga wote waliotajwa hawajawahi kutumia tarbia kuandika beti zaidi ya 50.
Na hakuna sehemu palipoandikwa na msomi au mtafiti yoyote wa Kiswahili k**a kuna uhuru wa kuvunja muundo wa shairi katika ushairi wa kimapokeo (ikiwa ni wa kisasa inafahamika wenyewe hauna ukomo wala mipaka katika jambo lolote).

Hoja ya “kutokujifunga” haikubaliki katika ushairi wa mapokeo, kwani kujifunga ndiko hutoa msingi wa sanaa yenyewe.
Mwisho nasisitiza mhalifu hawi kigezo cha kutokuwepo kwa sheria. Hoja ya sheria na kanuni hujibiwa kwa sheria na kanuni si rejea ya uhalifu wa muhalifu.

Nawakumbusha:
Vitakuro na viroja, vipo kwenye malumbano
Mtu akosapo hoja, huwa mwingi wa mifano
Mifano isonatija, na wingi wamatukano
Tujadili kwa hekima, watu wapate faida

MAREJELEO YA MAJIBU HAYA:

Abdulaziz, M.H. (1979). The History of Swahili Prosody. Nairobi: Kenya Literature Bureau.

Khamis, S.A. (2000). Ushairi wa Kiswahili: Nadharia na Misingi. Dar es Salaam: TUKI.

Mazrui, A. & Shariff, I. (1994). The Swahili: Idiom and Identity of an African People. Trenton: Africa World Press.

Mazrui, A. (1975). The Swahili Poetic Tradition. Nairobi: Heinemann.

Mulokozi, M. M. (1996). Theory and Practice of Swahili Poetry. Dar es Salaam: TUKI.

Shaban Robert (1954). Diwani ya Utenzi wa Vita vya Uhuru. Nairobi: East African Literature Bureau.

Wamitila, K.W. (2003). Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia. Nairobi: Focus Publishers.

Pichani*Mshairi mkongwe Mathias Mnyampala

ENDA OLEWAKashindwa kuja niamba, kule anapopajuwa,Ila kachukua namba, ya simu ile kajuwa,Kapiga na kuniamba, kwamba ames...
28/06/2025

ENDA OLEWA

Kashindwa kuja niamba, kule anapopajuwa,
Ila kachukua namba, ya simu ile kajuwa,
Kapiga na kuniamba, kwamba ameshachumbiwa,
Kasema enda olewa mimi anacha solemba.

K**a alijua kwamba, kwa hili sitamwelewa,
Nimeshindwa kumuomba, sababu ya kunitowa,
Maneno ameyakomba, kashaniacha mkiwa,
Kasema enda olewa mimi anacha solemba.

Ni k**a kakata kamba, nimeshachanganyikiwa,
Nimebakia kuimba, maneno niloambiwa,
"Eti nakwacha solemba, mie naenda olewa",
Kasema enda olewa mimi anacha solemba.

K**a kanipiga ndumba, kila siku ni makiwa,
Kwa jinsi alivyochamba, hadi nguvu naishiwa,
Kupenda tena nayumba, mateso yanizuzuwa,
Kasema enda olewa mimi anacha solemba.

Kwa sasa nacheza rumba, kitwani nishamtowa,
Mpaka sasa naamba, sababu hajaolewa,
Kichwani mambo naumba, mimi niliongopewa,
Kasema enda olewa mimi anacha solemba.

Mbona bado hana nyumba, yupo kwao amepowa,
Nini kilichomkumba, cha kuniacha mkiwa,
Yuwapi wake mchumba, kwangu aliyemwondowa,
Kasema enda olewa mimi anacha solemba.

Ningepiga yake namba, ya moyoni nikatowa,
Ila nakhofu ya kwamba, donda lisijeuguwa,
Nyuma kilichonikumba, kwangu kisijerudiwa,
Kasema enda olewa mimi anacha solemba.

Matozi mato yafumba, nashindwa kujing'atuwa,
Nakoma beti kuumba, karatasi imelowa,
Ni ngali bado mshamba, nguli penzini sijawa,
Kasema enda olewa mimi anacha solemba.

Mtunzi: Dadi Ntanila Ally
Lakabu: Zacash Wanolic
Mahali: Nyarutembo

MOFIMU HURU NA MOFIMU TEGEMEZI Understanding Swahili Morphemes: Free vs. BoundWelcome, Swahili learners! Today, we're di...
15/06/2025

MOFIMU HURU NA MOFIMU TEGEMEZI

Understanding Swahili Morphemes: Free vs. Bound
Welcome, Swahili learners! Today, we're diving into the fascinating world of morphemes – the smallest meaningful units of language. Understanding morphemes is crucial for grasping how Swahili words are built and how they carry meaning.
In Swahili, just like in many languages, morphemes can be categorized into two main types: mofimu huru (free morphemes) and mofimu tegemezi (bound morphemes).
1. Mofimu Huru (Free Morphemes)
A mofimu huru (free morpheme) is a morpheme that can stand alone as a complete word and still carry meaning. It doesn't need to be attached to another morpheme to make sense. Think of them as independent words.
Characteristics of Free Morphemes:
* They can be spoken alone.
* They have a clear dictionary meaning.
* They often form the root or base of a word.
Examples in Swahili:
| Swahili Free Morpheme | English Translation | Example Sentence (Swahili) | Example Sentence (English) |
|---|---|---|---|
| mtu | person | Mtu yule ni mrefu. | That person is tall. |
| kitabu | book | Nina kitabu kizuri. | I have a good book. |
| chakula | food | Chakula kiko tayari. | The food is ready. |
| na | and | Mimi na wewe. | Me and you. |
| lala | sleep | Watoto lala sasa. | The children sleep now. |
| kubwa | big | Nyumba ile ni kubwa. | That house is big. |
In the examples above, words like mtu, kitabu, chakula, na, lala, and kubwa can all stand by themselves and convey a complete meaning.
2. Mofimu Tegemezi (Bound Morphemes)
A mofimu tegemezi (bound morpheme) is a morpheme that cannot stand alone as a word. It must be attached to another morpheme (usually a free morpheme or another bound morpheme) to make sense and form a complete word. Think of them as "helpers" or "attachments."
Characteristics of Bound Morphemes:
* They cannot be spoken alone.
* They gain meaning only when attached to other morphemes.
* They often indicate tense, person, number, class, mood, or derivational changes.
Examples in Swahili:
Swahili is an agglutinative language, meaning words are often formed by adding many bound morphemes together.
| Swahili Bound Morpheme | Type/Function | Example Word (Swahili) | Breakdown | English Meaning of Word |
|---|---|---|---|---|
| a- | Subject Prefix (Class 1) | analala | a- (he/she) + -na- (present) + -lala (sleep) | He/She is sleeping |
| -li- | Past Tense Infix | alilala | a- (he/she) + -li- (past) + -lala (sleep) | He/She slept |
| tu- | Subject Prefix (1st person plural) | tunaimba | tu- (we) + -na- (present) + -imba (sing) | We are singing |
| -ni | Locative Suffix | dukani | duka (shop) + -ni (in/at) | in/at the shop |
| -ji | Reflexive Infix | ajipiga | a- (he/she) + -ji- (self) + -piga (hit) | He/She hit himself/herself |
| ki- | Noun Class Prefix (Class 7) | kitabu | ki- (noun class 7 prefix) + -tabu (root) | book |
| m- | Noun Class Prefix (Class 1) | mtu | m- (noun class 1 prefix) + -tu (root) | person |
Notice how morphemes like a-, -li-, tu-, -ni, -ji, ki-, and m- cannot stand alone. They only make sense when attached to a root or other morphemes to form a complete word.
Key Differences: Mofimu Huru vs. Mofimu Tegemezi
Let's summarize the main distinctions:
| Feature | Mofimu Huru (Free Morpheme) | Mofimu Tegemezi (Bound Morpheme) |
|---|---|---|
| Independence | Can stand alone as a word. | Cannot stand alone; must be attached to another morpheme. |
| Meaning | Has its own independent meaning. | Gains meaning only when attached; often modifies or adds grammatical information. |
| Examples | mtu (person), kitabu (book), lala (sleep) | -li- (past tense), a- (subject prefix), -ni (locative suffix) |
| Function | Forms the core meaning/root of a word. | Adds grammatical function, changes word class, or provides additional semantic detail. |
Exercise for Learners
Now, let's practice! For each of the Swahili words below, identify the morphemes and state whether they are mofimu huru (free morphemes) or mofimu tegemezi (bound morphemes). Explain your reasoning in English.
Example:
Word: Anasoma (He/She is reading)
* a-: Mofimu tegemezi (bound morpheme) - It's a subject prefix, cannot stand alone.
* -na-: Mofimu tegemezi (bound morpheme) - It's a tense infix, cannot stand alone.
* -soma: Mofimu huru (free morpheme) - It's the verb root 'read', can stand alone (e.g., 'soma' as an imperative).
Your Turn:
* Watoto
* morpheme(s) and type(s):
* reasoning:
* Walilala
* morpheme(s) and type(s):
* reasoning:
* Nyumbani
* morpheme(s) and type(s):
* reasoning:
* Kiti
* morpheme(s) and type(s):
* reasoning:
* Tunakula
* morpheme(s) and type(s):
* reasoning:
This lesson should help you differentiate between free and bound morphemes in Swahili. Keep practicing, and you'll soon master the structure of Swahili words! If you have any questions, feel free to ask.

MATUMIZI YA I & ME KATIKA LUGHAKatika lugha ya Kiswahili, sentensi ina pande kuu mbili ambazo ni Kiima na Kiarifu. Kiima...
11/06/2025

MATUMIZI YA I & ME KATIKA LUGHA

Katika lugha ya Kiswahili, sentensi ina pande kuu mbili ambazo ni Kiima na Kiarifu. Kiima ni upande ambao hukaliwa na mtendaji/watendaji wa kitendo. Na Kiarifu ni upande ambao hukaliwa kitendo(kitenzi) pia kitendwa (nomino inayopokea athari ya kitendo.

Hivyo, k**a unataka kutumia pronouns kwenye upande wa Kiima (mtenda/watendaji) basi pronouns hizi zitumike: She, he, it, I, you, we, they.
Mfano: She is eating ugali.
He learns English language.
It is raining at the moment.
I was watching TV.
You insulted Hadija.
We play football.
They are reading a book.

Pia k**a upande wa Kiima unapaswa kukaliwa na jina la mtu na kiwakulishi (pronoun), basi sheria inasema ni lazima uanze na jina kwanza kisha ifuate pronoun.
E.g
Juma and I are friends.
Asha and you are enemies.
Abdullah, Rashid, Neema and I will go to the party.

Upande wa Kiarifu.
Mabadiliko haya hutokea kwa upande wa pronouns:
I ---->me
You---->you
She--->her
He--->him
We--->us
They--->them
It--->it
Juma and I ---->us or Juma and me.
Mifano katika sentensi:
I saw her yesterday. (Uliyemuona jana ni wa k**e na anatambulika kwa jina na wazungumzaji husika)

My father chased him(mfukuzwa ni wa kiume)

She loves me (anayependwa ni nafsi ya kwanza umoja 'mimi')

We took them (waliochukuliwa ni wao)

They rejected us. (Waliokataliwa ni sisi)

She dislikes you. (Asiyependwa ni wewe / ninyi)

John na mimi tutakualika. (John and I will invite you.)

Utatualika John na mimi.(You will invite us. (Only if John is part of the conversation) or (You will invite John and me, if John is not part of the conversation.

Karibuni kwa michango zaidi.
Imeandikwa na Godfrey Mhaka

Address

Mafia
Dar Es Salaam

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Soma Kiswahili posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Contact The Establishment

Send a message to Soma Kiswahili:

Share

Category