18/05/2023
Kutoka 14:1-30 “…..Hata Farao alipokaribia, wana wa Israeli wakainua macho yao, na tazama, Wamisri wanakuja nyuma yao; wakaogopa sana; wana wa Israeli wakamlilia BWANA. Wakamwambia Musa, Je! Kwa sababu hapakuwa na makaburi katika Misri umetutoa huko ili tufe jangwani? Mbona umetutendea haya, kututoa katika nchi ya Misri? Neno hili silo tulilokuambia huko Misri, tukisema, Tuache tuwatumikie Wamisri? Maana ni afadhali kuwatumikia Wamisri kuliko kufa jangwani. Musa akawaambia watu, Msiogope, simameni tu, mkauone wokovu wa BWANA atakaowafanyia leo; kwa maana hao Wamisri mliowaona leo hamtawaona tena milele. BWANA atawapigania ninyi, nanyi mtanyamaza kimya. BWANA akamwambia Musa, Mbona unanililia mimi? Waambie wana wa Israeli waendelee mbele….”
Majaribu na changamoto zinapokujia unaongea nini? Wana wa Israeli majaribu yalipowajia waliwaza vifo, waliwaza mambo ya kale wakatamani kurudi kule Bwana alikowatoa wakajikuta wanaongea maneno hasi.
Wakati wa majaribu uwe makini sana maneno unayoongea kwani unaweza kujimaliza au kustawi. Katika majaribu na giza muite Mungu. Ukiwa gizani ukamuita Mungu maana yake unaita Nuru na utaona Njia ya kutoka.
Njia za Mungu hazichunguziki hivyo usimpangie Mungu kitu cha kukufanyia, Mungu ni Mungu MUWEZA wa yote na Asiyeshindwa na jambo lolote. Wana wa Israeli walipita katikati ya bahari ya Shamu na wakavuka salama hivyo basi na wewe ukimwamini Mungu utapita katikati ya maadui zako, katikati ya majaribu, aibu na shida na utavuka kwa Ushindi.
Mungu tunayemwabudu anaweza kufanya njia pasipokuwa na njia, ukipita katika majaribu tangaza njia kupatikana nayo mbingu ikisikia kuwa umetangaza hivyo itafanya njia hata pasipokuwa na njia.
©KUHANI ZEBEDAYO JACKSON SANGA - KANISA LA EFATHA SAYUNI - MOSHI KILIMANJARO.