19/12/2020
JIRANI (11)
ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA ....
"SIJISIKII vizuri,
Najihisi nina ngiri,
Acha nikanywe shubiri,
Naomba hapa bakia."
Beka akanitazama,
Kwa macho yenye huruma,
Kwa upole akasema,
Majibu kunipatia.
SASA ENDELEA....
"USIJALI sana kaka,
Mambo sawa nitaweka,
Kanywe dawa pumzika,
Hali nitakujulia.
K**a hali tazidi,
Usingoje sana hadi,
Uteteme kwa baridi,
Zahanati kimbilia.
K**a vipi nijulishe,
Nduguyo nikuwahishe,
Lisijezidi kasheshe,
Ugonjwa ukizidia.
Nilimsikiza vyema,
Nikamwonea huruma,
Moyoni hakunisoma,
Ukweli sikumwambia.
"Usijali naamini,
Nikishafika nyumbani,
Nitapata afueni,
Dawa nikishatumia.
"Sawa basi kaka nenda,
Usiogope k**anda,
Hili halitanishinda,
Amini nakuambia."
Tulipokubaliana,
Vizuri tukaagana,
Na yeye nikaachana,
Nami nikashika njia.
Nyumbani nikawasili,
Pote palikuwa tuli,
Ila watoto wawili,
Mlango walizuia.
Walikuwa wanacheza,
Mlangoni wamejaza,
Chupa za kuokoteza,
Hatari kuzitumia.
Ni vipande vyenye ncha,
Hovyohovyo wakiacha,
Miguu vitapekecha,
Majeraha kuwatia.
Ni Luka na Zainabu,
Watoto wenye adabu,
Licha ya zangu ghadhabu,
Wema niliwafanyia.
Nikachuchumaa kwao,
Huku ninasema nao,
Kuhusu mchezo wao,
Huku ninawatania.
"Luka na mchumba wako,
Hivi mmekosa jiko?
Oneni hapo mliko,
Mlangoni mwasikia?
Hapa mlipojiweka,
Peupe mnaoneka,
Wakiwazukia paka,
Pilau watawalia.
Wote wakatabasamu,
Kisha Luka kwa nidhamu,
"Akija nampa sumu,"
Kasema kuniambia.
Alinishangaza Luka,
Kauli alotamka,
Kichwani nikamshika,
Kisha nikamuambia.
"Sumu si kitu kizuri,
Epuka hii hatari,
Kuwa nayo 'sifikiri,
Ama utaangamia.
Luka mara akanena,
Machoye yamekazana,
"Wapi inapatikana?"
Swali akanitupia.
ITAENDELEA...