28/05/2026
Sehemu ya 15
Mzee Kazi alimtazama Jimmy kwa utulivu wa ajabu, kana kwamba alikuwa anatazama sinema ambayo tayari anajua mwisho wake. Aligeuka kumlenga Zawadi kwa jicho moja, kisha akasogeza mguu wake kuelekea upande wa meza ya mbao.
“Jimmy, mwanangu,” Kazi alisema kwa sauti ya chini, “Unajua kwanini nilikupenda kuliko watoto wa kaka zangu wote? Ni kwa sababu una tamaa ileile niliyokuwa nayo mimi ujanani. Lakini kuna kitu kimoja hukujifunza: Shamba hili halina mlinzi getini kwa sababu mlinzi wake yuko ndani ya kuta hizi.”
“Acha porojo! Fungua!” Jimmy alipiga kelele.
Kazi alibonyeza kwa kisigino chake sehemu fulani ya sakafu iliyokuwa imejificha chini ya zulia. Ghafla, sauti ya kimekanika ya click ilisikika. Sehemu ya sakafu ilisogea, ikionyesha sanduku dogo la chuma (safe) lenye vioo vya kidijitali.
“Sogeza kidole chako hapa, Ami,” Jimmy aliamuru, akimsukuma Kazi kuelekea kwenye lile sanduku.
Wakati Jimmy akielekeza macho yake yote kwenye lile sanduku, Zawadi alijua huu ndio wakati pekee wa kuchukua hatua. Alinyakua simu ya Mzee Kazi iliyokuwa juu ya meza. Aliona ‘app’ moja iliyokuwa wazi yenye maandishi mekundu: “SILENT DEFENSE”.
Zawadi hakusita. Alibonyeza kitufe cha “ACTIVATE”.
Ghafla, taa zote za ndani ya nyumba zilizima. Katika giza lile nene, milango ya chuma ya dharura ilishuka kwa kishindo kikubwa (BAM! BAM! BAM!), ikiziba madirisha na milango yote ya kutokea. Nyumba ikageuka kuwa gereza la chuma ndani ya sekunde tano.
“Nini hiki?” Jimmy alipiga kelele, akifyatua risasi moja hewani kwa hofu. Mwanga wa risasi ile ulimulika kwa sekunde moja, ukionyesha kivuli cha Mzee Kazi kikisogea kwa kasi.
“Zawadi! Lala chini!” Sauti ya Mzee Kazi ilisikika kutoka upande wa pili wa chumba.
Ghafla, mfumo wa kuzima moto wa nyumba ulianza kutoa gesi nyeupe yenye harufu kali ya kemikali. Haikuwa maji; ilikuwa gesi ya kulevya (tear gas/knock-out gas) inayotumika kudhibiti wahalifu.
“Pumbavu!” Jimmy alikohoa, akijaribu kufunika pua yake kwa shati, lakini nguvu zilianza kumuishia. Alijaribu kumlenga Mzee Juma, lakini giza na gesi vilimfanya akose mwelekeo. Bastola ilianguka sakafuni kwa mlio wa chuma.
Zawadi alijifunika pua yake kwa kanga, akimkumbatia mwanawe kwa nguvu sakafuni, akijaribu kutovuta hewa ile nzito. Alisikia vishindo vya miguu vikiingia kupitia mlango wa siri uliokuwa nyuma ya rafu ya vitabu.
Watu wanne waliovalia ‘Gas Masks’ na sare nyeusi waliingia. Hawakuwa polisi wa kawaida; walikuwa walinzi binafsi wa Mzee Kazi waliokuwa wamejificha shambani kwa siku zote hizo.
“Mk**ateni,” sauti ya Mzee Kazi iliamuru, safari hii ikiwa na mamlaka kamili. “Na msaidieni kaka yangu Juma, anaweza kuwa amevuta gesi nyingi.”
Alfajiri Inachomoza
Baada ya nusu saa, gesi ilikuwa imesafishwa na mfumo wa hewa. Taa zilikuwa zimewaka tena. Jimmy alikuwa amefungwa pingu mikononi na miguuni, akiwa ameketi sakafuni huku akitazama chini kwa aibu na chuki.
Mzee Juma alikuwa ameketi kwenye kochi, akipewa maji na mmoja wa walinzi, huku akimtazama Jimmy kwa machozi. “Jimmy... kwa nini? Tulikupa kila kitu.”
Mzee Kazi alisimama mbele ya Zawadi. Alichukua lile sanduku la chuma na kulifungua kwa urahisi—halikuhitaji hata alama ya kidole, lilikuwa tayari limefunguliwa. Ndani yake hamkuwa na almasi. Kulikuwa na bahasha moja tu ya khaki.
“Zawadi,” Kazi alisema, akimkabidhi ile bahasha. “Hapa ndani kuna hati za umiliki wa shamba hili na akaunti zangu zote za nje ya nchi. Siyo kwa jina langu, wala siyo kwa jina la Maria.”
Zawadi aliifungua bahasha ile. Macho yake yalijawa na machozi alipoona jina lililoandikwa kwenye nyaraka zote: KAZI MERIKION PASCAL (JUNIOR).
“Mwanangu?” Zawadi alinong’ona.
“Niliishi maisha ya uongo kwa miaka mingi, Zawadi,” Mzee Kazi alisema, akimgusa kichwa mwanawe. “Niliwasaliti watu wengi, ikiwemo kaka yangu Oscar. Lakini nilipokuona wewe kijijini, nilijua nimepata nafasi ya kurekebisha makosa yangu kupitia huyu mtoto. Almasi za kweli siyo mawe yaliyo chini ya ardhi; ni damu yangu iliyo safi.”
Ghafla, mlio wa helikopta ulisikika nje ya shamba.
“Nenda, Zawadi,” Kazi alisema kwa haraka. “Walinzi wangu watakuchukua wewe, mwanangu, na Ami Juma mpaka mahali salama nje ya nchi. Serikali itakuja hapa muda si mrefu, na lazima nikabiliane na makosa yangu ya zamani pamoja na Oscar na Mollel.”
“Wewe utafanya nini, Kazi?” Zawadi aliuliza, akimshika mkono.
Kazi alitabasamu, tabasamu lilelile la picha ya sebuleni Masaki, lakini safari hii lilikuwa na ukweli. “Nitakaa hapa nimsubiri mdogo wangu Oscar. Safari hii, hatutapambana k**a maadui. Nitamkabidhi ushahidi wote utakaomtoa gerezani na kumfanya awe mtu huru, mradi tu akubali kumlinda mwanangu akirejea hapa miaka ijayo.”