08/03/2026
Salva Africa TV Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma, amekutana na msanii wa muziki wa Bongo Fleva Mac Voice ili kusikiliza malalamiko yake kuhusiana na mgogoro wake na msanii na mmiliki wa lebo ya muziki ya Next Level Music, Rayvanny.
Mazungumzo hayo yalifanyika katika Ofisi za Wizara hiyo zilizopo Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam Machi 6, 2026, ambapo Naibu Waziri alisema Serikali imeanza kuchukua hatua za kufuatilia sakata hilo ili kupata ukweli wa madai yaliyotolewa na pande husika, huku akiahidi kuwa suala hilo litafanyiwa kazi haraka ili kupata ufumbuzi wa haki kwa pande zinazohusika.
Mgogoro kati ya Mac Voice na Rayvanny umeibuka baada ya msanii huyo kudai kuwa hakupokea malipo ya kazi yake akiwa chini ya Lebo ya Next Level Music, licha ya makubaliano ya mgawanyo wa mapato yaliyofikiwa wakati wa kusaini mkataba huo.
Sakata hilo limezua mjadala mkubwa kwenye mitandao ya kijamii na kwa wadau wa muziki nchini. Mhe. Mwinjuma alieleza kuwa Serikali ina wajibu wa kuhakikisha haki na maslahi ya wasanii yanaheshimiwa huku akisisitiza umuhimu wa kuwepo kwa mikataba ya wazi na yenye kulindana katika sekta ya sanaa.
Kwa upande wake Mac Voice alimshukuru Naibu Waziri kwa kuonyesha nia ya kusikiliza kero zake na kuahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa mamlaka husika ili suala hilo liweze kutatuliwa.
#1